JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


BENKI YA CRDB YASHINDA TUZO YA UBORA WA HUDUMA YA ESQR 2024

Share This
Mkuu wa Huduma kwa Wateja Benki ya CRDB, Yolanda Uriyo (wa pili kushoto) akipokea Tuzo ya Ubora wa Huduma ya mwaka kutoka kwa Michael Harris, Mkurugenzi Mtendaji wa Jumuiya ya Utafiti wa Ubora ya Ulaya (ESQR). Wanaotazama ni Mwakilishi kutoka Ubalozi wa Tanzania Brussels, Vivian Rutaihwa (wa kwanza kulia), na Meneja Mwandamizi wa Uhakiki wa Ubora wa Huduma wa Benki hiyo, Mshindo Magimba.
 
======   ======
 
 Brussels, 30 Julai, 2024 - Benki ya CRDB imetunukiwa Tuzo ya Ubora wa Huduma kwa mwaka 2024 na Jumuiya ya Ulaya ya Utafiti wa Ubora (ESQR) katika hafla ya utoaji wa tuzo iliyofanyika katika hoteli ya Le Plaza katika jiji la Brussels, Ubelgiji.

Tuzo hiyo ilitolewa kwa kutambua jitihada za Benki hiyo katika kuboresha usimamizi wa ubora katika huduma zake zote. Tuzo ambazo zinafanyika kila mwaka zinatambua taasisi na mashirika ambayo yamewekeza katika huduma ubora kwa wateja katika sekta mbalimbali, ikiwamo sekta ya fedha kote ulimwenguni.
Benki ya CRDB imekuwa ikiwekeza kwa kiasi kikubwa katika mifumo ya utoaji huduma bora inayojumuisha teknolojia za kisasa ili kutoa uzoefu bora katika kila hatua ya safari ya mteja. Ushindi wa tuzo hii, unathibitisha namna gani Benki ya CRDB imekuwa mshirika mzuri kwa wateja na wadau wake, ikichangizwa na wafanyakazi wenye weledi mkubwa ambao wamekuwa wakiwapa wateja suluhisho bora na zinazoendana na mahitaji yao halisi.

Akizungumzia wakati wa hafala ya kupokea tuzo hiyo Mkuu wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja, Yolanda Uriyo, alisema, "Mtazamo wetu kubuni njia bora za kuwahudumia wateja umekuwa ndio msingi wa mafanikio yetu ya katika nyanja ya huduma kwa wateja na usimamizi wa ubora. Tuzo hii ni ushahidi wa bidii ya timu yetu katika kutoa huduma bora kwa wateja wetu.”

Aliongeza kuwa tuzo hiyo inaakisi maono ya kimkakati ya Benki ya CRDB chini ya mkakati wake mpya wa muda wa kati, 'Evolve,' unaojumuisha mipango mbalimbali ya huduma kwa wateja inayolenga kuboresha utoaji wa huduma. Mipango hii imeimarisha nafasi ya Benki ya CRDB katika soko huku ikiimarisha uhusiano na wateja na ufanisi wa kiutendaji.
Akizungumza kuhusu tuzo hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela, alisema kutambuliwa na ESQR ni hatua muhimu inayosisitiza dhamira ya Benki katika ubora na umahiri katika shughuli zake zote. "Juhudi za timu yetu katika uvumbuzi na mbinu zinazomjali mteja zinaendelea kututofautisha katika sekta ya benki. Tunaendelea kujidhatiti katika kuinua viwango vyetu vya huduma na kutoa thamani endelevu kwa wateja na wadau wetu," aliongeza.

Mbinu bunifu zilizochangia tuzo hiyo ni pamoja na utekelezaji wa mifumo ya kidijitali ya maoni ya wateja kama vile misimbomilia (QR Code) na mfumo wa jumbe fupi (SMS), zilizopelekea kuwapa wateja njia rahisi za kutoa maoni na kuwezesha benki kushughulikia kwa haraka. Zaidi ya hayo, Benki hiyo imekuwa ikifanya tathmini za mara kwa mara za ubora wa huduma na utoaji wa bidhaa, kuhakikisha uboreshaji endelevu na kuvuka matarajio ya wateja.

Akiwa ameongozana na Ujumbe wa Benki ya CRDB, Mwakilishi wa Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji, Vivian Rutaihwa, alitipongeza Benki ya CRDB kwa kushinda tuzo hiyo akisema inaleta sifa nzuri sit u kwa benki hata Taifa kwa ujumla, “Tunajisikia fahari kubwa kuona Benki ya CRDB inatambulika kimataifa kwa huduma ubora ikitoa taswira ya viwango vya huduma kwetu kama nchi. Tunatamani kuona taasisi nyingi zikifikia viwango hivi."
Naye Michael Harris, Mshauri Mkurugenzi Mtendaji wa ESQR, aliipongeza Benki ya CRDB kwa mafanikio yake na kubainisha, "Ushindi wa tatu wa Benki ya CRDB wa Tuzo ya Ubora wa Huduma ni kielelezo cha dhamira yake isiyoyumba ya ubora na ubunifu katika huduma za kibenki. Tunawapongeza kwa kujitolea kwao kuweka viwango vya ubora wa usimamizi."

Hii ni mara ya tatu kwa Benki ya CRDB kutunukiwa tuzo ya ubora ya ESQR. Tangu Januari 2024, Benki hiyo imepata tuzo kubwa 26, ikiwa ni pamoja na Benki Bora Tanzania katika Tuzo za Global Finance, Benki Bora ya Biashara Tanzania katika Tuzo za International Banker, Benki Bora ya Ubunifu wa Huduma Inayomjali Mteja Tanzania katika Tuzo za Global Brands, na Benki Bora ya Ubunifu Tanzania katika Tuzo za Gazette International.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad