Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Uwanja wa Arusha, utakaotumika katika michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2027 (AFCON 2027), unaojengwa Jijini Arusha.
Makamu wa Rais amepongeza maendeleo ya ujenzi wa uwanja huo, ambapo amesema ni faraja kuona ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa ili kuvutia michuano hiyo kufanyika nchini Tanzania, inatakelezwa kikamilifu. Amemshukuru Mhe. Rais kwa kuendelea kutoa fedha ili kuhakikisha uwanja huo unakamilika kwa wakati.
Aidha, Makamu wa Rais ameishukuru Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na mkoa wa Arusha, Wakandarasi na Mshauri Elekezi kwa kazi kubwa waliyofanya katika Uwanja huo.
Makamu wa Rais amewataka Viongozi wa Wizara pamoja na Mkoa wa Arusha kusimamia vema agizo la Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan la kuhakikisha barabara zinazotumika katika kufika uwanjani hapo zinakamilika kwa wakati.
Awali Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Amos Makala, amemueleza Makamu wa Rais, maendeleo ya ujenzi wa uwanja huo ambao umefikia asilimia 88, ukitarajiwa kukamilika ifikapo mwishoni mwa mwezi Agosti, 2026.
Uwanja wa Arusha, utakapokamilika, mbali na michezo, unatarajiwa kuwa kivutio cha utalii ukiwa umebeba alama ya Mlima Kilimanjaro, Madini ya Tanzanite na Bendera ya Taifa.













No comments:
Post a Comment