Katika kuunga Mkono jitihada za Serikali za kukuza shughuli za ufugaji nchini, Benki ya NMB imesaini makubaliano ya udhamini wa miaka mitatu kwaajili ya maonesho ya Mifugo ya Kimataifa (Tri-Nations Livestock Expo 2026-2028) ambayo yatashirikisha wafugaji kutoka nchi za Tanzania, Kenya na Namibia.
Maonesho haya ya mifugo hufanyika kila mwaka, na kwa mwaka huu, yatafanyika kuanzia Juni 19 hadi 21 Ubena Zomozi – Chalinze mkoani Pwani.
Mkuu wa Idara ya Kilimo Biashara wa Benki ya NMB, Nsolo Mlozi alisema kuwa Benki ya NMB inajivunia mafanikio makubwa ya maonesho hayo katika miaka miwili ya 2024 na 2025, yaliyoisukuma Benki hiyo kuboresha mkataba mpya aliouita ‘Uwekezaji wa Kimkakati.’
“Mkataba huu ni uwekezaji wa kimkakati unalenga kukuza sekta ya ufugaji na kuboresha maisha ya Watanzania wanaojihusisha na Sekta ya Kilimo - mnyororo wa thamani unaojumuisha kilimo chenyewe, uvuvi na ufugaji,” alisema Mlozi akibainisha kuwa hadi 2025 NMB ilikuwa imekopesha zaidi ya Sh. Bil. 100.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mbogo Ranches, Naweed Bulla, aliishukuru NMB kwa kukubali kudhamini kwa dau nono maonesho hayo, huku Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dr. Fabian Madele akisema kua ushirikiano baina ya Mbogo Ranches na NMB utakuza zaidi maonesho hayo na kuahidi kuwaunga mkono katika miaka mitatu ya mkataba huo.
Maonesho ya Tri-Nations Livestock Expo ni jukwaa muhimu la ushirikiano, ubunifu na biashara linalowezesha kiuchumi wafugaji na wadau wake wote, ambao watanufaika kupitia mbinu bora za ufugaji, elimu ya bima, mikopo, sambamba na kuyafikia masoko ya kitaifa na kimataifa.




No comments:
Post a Comment