JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


BASHE: MFUMO WA TMX NDIYO MWELEKEO

Share This

 







SERIKALI imeanza kutumia mfumo wa Soko la Bidhaa Tanzania (TMX) kwa zao la Korosho kwa msimu wa mauzo mwaka huu unaoanza hivi karibuni ili kumlinda mkulima kwa kupokea malipo moja kwa moja kutoka kwa Vyama Vikuu vya Ushirika badala ya mzunguko kupitia Vyama vya Msingi (AMCOS).

“Ni Lazima tuwe na mfumo imara wa kujua zao limezalishwa na nani, eneo gani na ubora wake (traceability) ili kuendana na soko la kimataifa kwa wakulima wa korosho. Mfumo wa TMX na Commodity Market Exchange ni suluhisho linalohitajika na tutaendelea kuboresha mfumo kadri inavyohitajika,” amesema Waziri wa Kilimo Mhe. Hussein Bashe (Mb) wakati wa Mkutano na Wadau wa Korosho kuelekea Msimu wa Mauzo ya Korosho mkoani Mtwara, tarehe 30 Septemba 2024.

TMX ni mfumo unaosimamia mnada wa kijiditali kwa lengo la kuwaongezea uhakika wa masoko, uhuru wa kuamua bei, uhakika wa malipo yao pamoja na kuchochea ushindani kwa mazao ya wakulima nchini.

“Vitu ambavyo tuna uwezo navyo kama wakulima ni ubora wa mazao, tija ya uzalishaji, na hilo linafungua soko imara kwa mazao yetu. Tija na ubora ndivyo vitaleta bei nzuri kwenye masoko,” amesema Waziri Bashe.

Ametolea mfano uzalishaji wa Korosho kwa mwaka 2022/2023 ulikuwa laki 189,000 ambapo msimu uliopita umeongezeka hadi laki 310,000; ambalo ni ongezeko la takribani tani 120,000.

Mkurugenzi wa Bodi ya Korosho, Bw. Alfred Francis amesema kuwa mfumo wa TMX umeendelea kuboreshwa kwa kushirikiana na Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA). “Tumepanga pia kutoa mafunzo ya mauzo ya Korosho kwa kutumia mfumo wa TMX demo ili wauzaji na wanunuzi wapate elimu kabla ya kuanza matumizi yake wakati wa msimu wa mauzo,” ameeleza Mkurugenzi Francis.

Bw. Yusuph Nanyila, Rais wa Korosho amesema kuwa zao la Korosho ni moja ya mazao ya kimkakati ambalo pia kwa upendeleo wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan wakulima wamekuwa wanapata pembejeo kusaidia uzalishaji wa zao hilo. “Kwenye maendeleo kuna changamoto lakini kusema ukweli tamko la Mhe. Rais kusema kuwa wakulima wataanza kulipwa moja kwa moja na Vyama Vikuu vya Ushirika lilikuwa la kheri kwa wakulima,” ameongeza Bw. Nanyila.

Mkutano huo pia umeshirikisha Mhe. Kanali Patrick Sawala, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mhe. Zainab Telack, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, wafanyabiashara, wawekezaji, wasafirishaji wa zao la Korosho.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad