JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


Tume ya Madini yatahadharisha waombaji leseni

Share This







• Yawataka kuzingatia sheria
TUME ya Madini katika kuhakikisha wananchi wananufaika na rasilimali madini, imeendelea kutoa huduma kwa wazawa ya kuwasajili katika mfumo wa uombaji leseni mtandaoni huku wakitahadharishwa kuzingatia sheria ya madini ili wasipoteze sifa za kumiliki leseni.

Huduma hiyo inatolewa katika Banda la Tume ya Madini kwenye Maonesho ya 48 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam 'Sabasaba' yanayofikia tamati kesho.

Mhandisi Daniel Mdachi akizungumza leo Julai 12, 2024 amesema Tume ya Madini inasimamia shughuli zote za utoaji wa leseni za uchimbaji na biashara ya madini, mipango ya ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (LCPs) kutoka kwa Wamiliki na Waombaji wa leseni za madini pamoja na watoa huduma kama takwa mojawapo la Sheria ya Madini Sura ya 123.

Amesema, waombaji leseni ni sharti kuzingatia sheria ya madini sura ya 123 ili kuepuka kufutiwa leseni na kuepuka kupoteza sifa za kumiliki leseni.

Mhandisi Mdachi amesema wapo wananchi wanaomba leseni lakini hawalipi ada stahiki, wengine hawawasilishi nyaraka muhimu.

Mdachi amesema ili mtu awe na sifa za kuomba leseni ni lazima azingatie Sheria ya Madini na kanuni zake.

Ambapo ameeleza kuwa kuna makundi mbalimbali ya leseni za madini ambazo ni leseni za uchimbaji mdogo, leseni za utafiti, Leseni za uchimbaji wa kati, Leseni za uchimbaji mkubwa na Leseni za uchenjuaji, uyeyushaji na usafishaji wa madini.

Amesema leseni za uchimbaji mdogo hutolewa kwa watanzania pekee waliokidhi vigezo kwa mujibu wa Sheria ya Madini wakati leseni za utafiti zinatolewa kwa wageni au wazawa kwa ajili ya mwekezaji kufanya utafiti na kubaini uwepo wa mashapo yanayoweza kuchimbwa kwa faida.

“Baada ya kujiridhisha uwepo wa mashapo yanayoweza kuchimbwa kwa faida ataomba Leseni ya uchimbaji: uchimbaji wa kati (ML) au Uchimbaji mkubwa (SML) kulingana na ukubwa wa mtaji wa uwekezaji,”amesema na kuongeza,

“Mwekezaji anayeomba leseni ya uchimbaji wa kati au mkubwa anatakiwa kuambatisha cheti cha mazingira ‘Environmental and Social Impacts Certificate’, Taarifa ya upembuzi yakinifu –‘Feasibility Study’, mpango wa ushirikishwaji wa watanzania kwenye uchimbaji, mpango wa fidia na uhamishaji wa makazi, uthibitisho wa utaalam na fedha,”amesema.

Aidha, Mdachi amesema leseni za biashara ya madini zipo za aina mbili:Leseni ndogo (Brokers) za biashara na leseni kubwa (Dealers) za biashara ya madini.

Amesema leseni ndogo za biashara hutolewa kwa watanzania pekee waliokidhi vigezo kwa mujibu wa Sheria ya Madini Sura ya 123.

Pia, leseni kubwa za biashara ya madini hutolewa kwa wazawa au wazawa na wageni wenye kampuni ambapo mzwa ana hisa zisizopungua asilimia 25.

Imeelezwa kuwa uhai wa leseni za biashara ya madini ni miezi kumi na mbili kuanzia tarehe 1 Julai hadi tarehe 30 Juni ya mwaka unaofuata.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad