JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


NBC Yasisitiza Dhamira Yake Kuchochea Ustawi Biashara kati ya Tanzania na Afrika Kusini.

Share This

 BENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) imesisitiza kuhusu dhamira yake ya kufanikisha ustawi wa biashara baina ya Tanzania na Afrika kusini kwa kuwawezesha wafanyabiashara wa mataifa hayo mawili ili waweze kupanua zaidi biashara zao sambamba na kuchangamkia fursa zaidi nje ya mipaka ya nchi hizo kufuatia hatua ya Umoja wa Africa kujumuishwa kuwa mwanachama wa kudumu katika muungano wa Umoja wa bara Ulaya G-20.

Dhamira hiyo imewekwa bayana na Mkurugenzi wa Hazina na Masoko ya Fedha wa Benki ya NBC Bw Peter Nalitolela wakati akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo Bw Theobald Sabi kwenye Mkutano wa Jukwaa la Wafanyabiashara wa Afrika Kusini nchini Tanzania uliofanyika jijini Dar es Salaam jana jioni ukihudhuriwa pia Balozi wa Afrika Kusini hapa Tanzania Bi Noluthando Malepe.

Kwa mujibu wa Bw Nalitolela, kupitia huduma zake mbalimbali za kifedha ikiwemo mikopo ya ukuzaji mitaji, dhamana, huduma ya fedha za kigeni sambamba na huduma ya malipo kwa njia ya mtandao inayofahamika kama ‘NBC Connect’ benki hiyo imedhamiria kurahisisha zaidi ufanisi wa biashara kwa wafanyabiashara wa mataifa hayo ili waweze kushiriki kwa ushindani zaidi kwenye fursa hiyo mpya ya kimataifa.

“Tumefurahi kuona kwamba Mheshimiwa Balozi wa Afrika Kusini hapa Tanzania Bi Noluthando Malepe nae amewasisitiza wafanyabiashara kuchangamkia soko hili jipya la G -20 nasi NBC pia tunawathibitishia kuwa tupo tayari Kwenda nao bega kwa bega kufanikisha hili kupitia huduma zetu muhimu za kifedha ambazo zimebuniwa mahususi kurahisha mahitaji yao ikiwemo mikopo, dhamana, upatikanaji wa fedha za kigeni na zaidi huduma yetu ya malipo kwa njia ya mtandano yaani NBC Connect itakayowawezesha kufanya mihamala mbalimbali yakiwemo malipo ya serikali na tozo mbalimbali’’ alitaja.

Alisema kwa muda mrefu sasa benki hiyo imekuwa mdau mkubwa wa wafanyabiashara kati ya Afrika Kusini na Tanzania ambapo kupitia mkutano huo uliodhaminiwa na benki ya NBC, alitaja baadhi ya sekta zinazotazamwa zaidi na benki hiyo kuwa ni pamoja na sekta za kilimo, usafirishaji, mawasiliano, biashara na madini.

Awali akizungumza kwenye mkutano huo Balozi Noluthando Malepe aliitaja Tanzania kama moja ya nchi bora zaidi kwa uwekezaji kutokana na uwepo wa fursa nyingi za kibiashara huku akitaja uwepo wa amani nchini Tanzania pamoja na ushirikiano wa kihistoria uliodumu kwa muda mrefu baina ya Tanzania na Afrika Kusini kama nguzo muhimu katika kufanikisha ustawi wa biashara baina ya mataifa hayo mawili.

“Hivyo nawaomba sana muitumie vema fursa hii ya amani na ushirikiano tuliona nao na wenzetu wa Tanzania kustawisha biashara zenu. Popote mnapohisi kuna changamoto tunawakaribisha ofisi za ubalozi ili tuweze kujadili namna bora ya kuzitatua huku pia tukijadili fursa nyingine zaidi,’’ aliomba Balozi Malepe.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jukwaa la Wafanyabiashara wa Afrika Kusini nchini Tanzania, Bw Manish Thakrar alisema pamoja na mambo mengine, nia ya jukwaa hilo ni kuunga mkono jitihada za serikali katika kuvutia wawekezaji wengi zaidi kutoka nje ya nchi kuja kuwekeza nchini Tanzania, huku akitaja suala la upatikanaji wa huduma za kifedha za uhakika kama moja nguzzo muhimu katika kufanikisha agenda hiyo.

“Hata hivyo Habari njema ni kwamba ushirikiano wetu na benki ya NBC uliodumu kwa muda mrefu sasa umeendelea kutuhakikishia upatikanaji wa huduma bora za kifedha. Tumefarijika zaidi kusikia kwamba NBC wanaendelea kutuhamasisha kuhusu ushiriki wetu kwenye soko la G-20 huku wakituhakikisha ufanisi zaidi kwenye upatikanaji wa mitaji zaidi na huduma nyingine nyingi za kifedha,’’ alisema Bw Thakrar ambae pia lionyesha kuvutiwa zaidi na huduma ya malipo ya mtandao ya NBC Connect.

Mkurugenzi wa Hazina na Masoko ya Fedha wa Benki ya NBC Bw Peter Nalitolela akizungumza na wajumbe wa Jukwaa la Wafanyabiashara wa Afrika Kusini nchini Tanzania wakati wa mkutano wa jukwaa hilo ulifanyika jijini dar es salaam jana.

Balozi wa Afrika Kusini nchini Tanzania Bi Noluthando Malepe (alieshika kipaza sauti) akizungumza na wajumbe wa Jukwaa la Wafanyabiashara wa Afrika Kusini nchini Tanzania wakati wa mkutano wa jukwaa hilo ulifanyika jijini dar es salaam jana. Wanaomsikiliza ni Pamoja na Mwenyekiti wa Jukwaa hilo Bw Manish Thakrar (kushoto kwa balozi) pamoja na Mkurugenzi wa Hazina na Masoko ya Fedha wa Benki ya NBC Bw Peter Nalitolela (kushoto kwa Mwenyekiti)

Mkurugenzi wa Hazina na Masoko ya Fedha wa Benki ya NBC Bw Peter Nalitolela (Kushoto) akibadilishana mawazo na baadhi ya viongozi waandamizi  wa Jukwaa la Wafanyabiashara wa Afrika Kusini nchini Tanzania wakati wa mkutano wa jukwaa hilo ulifanyika jijini dar es salaam jana.

Balozi wa Afrika Kusini nchini Tanzania Bi Noluthando Malepe (wa tatu kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa Jukwaa la Wafanyabiashara wa Afrika Kusini nchini Tanzania wakiongozwa na Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo  Bw Manish Thakrar pamoja na  maofisa wa benki ya NBC wakiongozwa na Mkurugenzi wa Hazina na Masoko ya Fedha wa Benki ya NBC Bw Peter Nalitolela (wa tatu kushoto) wakati wa mkutano wa jukwaa hilo ulifanyika jijini dar es salaam jana.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad