JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


NI MARUFUKU WATOTO KUMILIKI LESENI ZA MADINI

Share This
Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya Kati Singida, Sosthenes Masolla (aliyesimama), akifungua semina kwa wachimbaji wadogo wa madini kuhusu mfumo mpya wa huduma za utoaji wa leseni za madini kwa njia ya mtandao. Semina hiyo ilifanyika mjini Singida Septemba 5, mwaka huu. Wengine pichani ni wataalamu kutoka Wizara ya Nishati na Madini. Kutoka kushoto ni Placid Kabyemera, Juma Masoud, Mhandisi Nuru Shabani, Mhandisi Gabriel Senge na Tantao Tantao.
 Sehemu ya washiriki wa semina kuhusu matumizi ya mfumo mpya wa huduma za utoaji wa leseni kwa njia ya mtandao iliyofanyika mjini Singida Septemba 5, mwaka huu. Semina hiyo ni mwendelezo wa zoezi la utoaji mafunzo kwa wachimbaji wadogo wa madini nchi nzima kuhusu matumizi ya huduma hiyo mpya.

Na Veronica Simba - Singida
Imeelezwa kuwa ni marufuku kwa watoto walio chini ya umri wa miaka 18 kuandikishwa kama wabia wa umiliki wa leseni za madini za aina yoyote hapa nchini.

Hayo yameelezwa hivi karibuni na Mtaalamu kutoka Wizara ya Nishati na Madini, Mhandisi Nuru Shabani wakati wa semina kwa wachimbaji wadogo wa madini mkoani Singida kuhusu matumizi ya mfumo mpya wa huduma za utoaji leseni za madini kwa njia ya mtandao ujulikanao kama OMCTP (Online Mining Cadastre Transactional Portal.)

 “Sheria hairuhusu kutoa leseni kwa watoto walio chini ya umri wa miaka 18 na kwa wale watakaobainika kutoa taarifa zisizo za kweli kwa kuwaandikisha watoto walio chini ya umri husika kama wabia wa umiliki wa leseni za madini, watachukuliwa hatua kali za kisheria,” alisema Mhandisi Shabani.

Aidha, Mhandisi Shabani aliwataka washiriki wa semina hiyo na watanzania wote kwa ujumla kufahamu kuwa ni Wizara ya Nishati na Madini pekee ndiyo yenye mamlaka ya kutoa leseni za madini za aina zote hapa nchini.
Alitoa ufafanuzi huo baada ya baadhi ya washiriki wa semina kuuliza iwapo kuna mamlaka nyingine nchini zinazoruhusiwa kisheria kutoa leseni za madini.

“Kuna baadhi ya watu au vikundi vya watu au taasisi ambazo zimekuwa zikiingilia zoezi la utoaji wa leseni za madini kwa baadhi ya waombaji nchini. Naamini wanafanya hivyo kwa kutokujua sheria, hivyo ni vyema watu wote wafahamu kuwa hakuna mamlaka nyingine hapa nchini yenye ruhusa ya kutoa leseni za madini kisheria isipokuwa Wizara ya Nishati na Madini pekee,” alisisitiza.

Mhandisi Shabani aliwataka wananchi hasa wamiliki halali wa leseni za madini wanaokumbana na matatizo ya kutotendewa haki kwa kuzuiliwa kuendesha shughuli zao katika maeneo yao kisheria, kutoa taarifa kwa ofisi za madini zilizopo karibu naoi li waweze kupatiwa msaada kwa kufuata sheria.

Pia, aliwaasa wachimbaji madini wadogo na wamiliki wa leseni pamoja na wananchi wote hususani viongozi wa vijiji, halmashauri na taasisi mbalimbali, kuisoma na kuifahamu Sheria ya Madini ya mwaka 2010 ili kuepusha migogoro mbalimbali inayotokea kuhusiana na shughuli za uchimbaji wa madini.

Semina iliyofanyika Singida kwa wachimbaji wadogo wa madini kuhusu matumizi ya mfumo mpya wa huduma za utoaji wa leseni za madini kwa njia ya mtandao, ni mwendelezo wa mafunzo yanayoendelea kutolewa kwa wachimbaji wadogo nchi nzima chini ya Wizara ya Nishati na Madini kwa lengo la kuongeza uwazi na kuboresha zaidi huduma za sekta ya madini.

Washiriki mbalimbali wa semina kuhusu matumizi ya mfumo mpya wa huduma za utoaji wa leseni kwa njia ya mtandao, wakiuliza maswali wakati wa semina hiyo. Semina ilifanyika mjini Singida Septemba 5, mwaka huu.
 Mhandisi Migodi kutoka Wizara ya Nishati na Madini, Nuru Shabani, akiwasilisha mada mbalimbali kuhusu matumizi ya mfumo mpya wa huduma za utoaji leseni za madini kwa njia ya mtandao (Online Mining Cadastre Transactional Portal – OMCTP) kwa Wachimbaji madini wadogo, wakati wa Semina maalumu iliyofanyika Septemba 5, mwaka huu mjini Singida.
Viongozi na wataalamu kutoka Wizara ya Nishati na Madini, wakiwa katika picha ya pamoja na wachimbaji wadogo wa madini kutoka mkoani Singida walioshiriki katika Semina kuhusu matumizi ya mfumo mpya wa huduma za utoaji wa leseni kwa njia ya mtandao. Wa tatu kutoka kulia (Waliokaa kwenye viti) ni Kamishna Msaidizi wa Madini wa Kanda ya Kati – Singida na Kulia kwake ni Mhandisi Migodi kutoka Wizara ya Nishati na Madini, Nuru Shabani. Semina ilifanyika Septemba 5, mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad