Watu wengi wamenunua viwanja/nyumba lakini mali hizo zimeendelea
kubaki katika majina ya waliowauzia. Wapo ambao imepita hata
miaka kumi tangu wanunue maeneo lakini bado hawajabadili jina
kuingia jina lake. Zipo sababu nyingi zinazosababisha hali hiyo lakini
moja ni watu kutokujua umuhimu wa kubadili jina kwa haraka.
Hapa sizungumzii tu kubadili jina isipokuwa nazungumzia kubadili
jina kwa haraka. Kupitia makala haya napenda kuwaamsha watu
kuhusu umuhimu mkubwa wa kubadili jina kwa haraka iwapo
umenunua nyumba/kiwanja kwa mtu. Ni muhimu sana kufanya
hivyo na itakuepusha na mambo mengi.
1.KAMA HUJABADILI JINA ALIYEKUUZIA BADO NDIYE MMILIKI.
Ikiwa kutatokea mgogoro wa umiliki wakati ambao umenunua
nyumba/kiwanja na hujabadili jina kwenda kwenye jina lako kuna
hatari kubwa zaidi ya kupoteza ulichonunua. Hii ni kutokana na
ukweli kuwa utapokuwa unatatuliwa mgogoro wa nani mmiliki swali
la kwanza huwa ni nani ambaye nyaraka ya umiliki ina jina lake.
Yule ambaye jina lake linaonekana kwenye hati au leseni ya makazi
ndiye hupewa kipaumbele na kwa mujibu wa sheria mwenye jina
kwenye hati au leseni ya makazi ndiye mmiliki. Wewe uliyenunua
utakuwa na mkataba na jina lako litakuwa kwenye mkataba lakini
pamoja na kuwa na jina kwenye mkataba bado huwezi kulinganisha
mkataba na hati au leseni ya makazi. Jina linalotokea kwenye hati
au leseni ya makazi huwa na nguvu zaidi kuliko lile la kwenye
mkataba.


No comments:
Post a Comment