JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


TANZANIA YAHIMIZA USHIRIKIANO KATIKA KUWASAIDIA WAKIMBIZI

Share This
 Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon,  akizungumza wakati wa  Mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu dhana ya wajibu wa kuwalinda raia, ambapo alisema licha ya kuasisiwa kwa dhana hiyo dunia bado imeendelea kushuhudia  maisha ya watu wasiokuwa na hatia yakiendelea kupotea  kwa sababu tu Jumuiya ya Kimataifa inashindwa kutumiza wajibu wake kwa wakati.
 Balozi Tuvako Manongi akizungumza wakati wa Majadiliano ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu  dhana ya kuwalinda raia (R2P) majadiliano yaliyojielekeza katika kutathimini mafanikio na changamoto za utekelezi wa dhana hiyo ikiwa ni miaka kumi tangu kuasisiwa  kwake.
 Picha hii  ya maktaba ni ya  wakimbizi  katika kambi moja nchini Tanzania,  ambao jana  jumanne akizungumza katika Mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa,  Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika UN Balozi Tuvako Manongi amesema kutoka na wimbi kubwa linaloendelea la wakimbizi  kukimbilia mataifa mengine kutafuta usalama wao. Jumuiya ya kimataifa haina budi kushirikiana na bila  kubagua katika  kuwalinda na  utoaji wa huduma na misaada ya kibinadamu kwa wakimbizi.

Na Mwandishi Maalum,  New York
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  imetoa wito kwa   Jumuiya ya Kimataifa wa kushirikiana katika  wajibu wa kuwalinda na kuwapatia misaada ya kibinadamu,  wakimbizi wanaokimbia machafuko, vita na  migogoro katika nchi zao.
Wito huo  umetolewa   siku  ya jumanne na Balozi Tuvako Manongi,Mwakilishi wa  Kudumu  wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa,   wakati  Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa,  lilipokutana  kwa majadiliano  ya  siku moja kuhusu utekelezaji wa dhana juu ya wajibu wa kulinda raia (R2P) mafanikio na changamoto zake.

Dhana  ya wajibu wa kuwalinda raia  dhidi ya  mauaji ya kimbari, uhalifu wa kivita,  mauaji ya kikabila na uhalifu dhidi ya  binadamu   ilianzishwa mwaka 2005 wakati  wa mkutano wa Kimataifa  uliofanyika mwaka huu, ambapo viongozi wakuu  wa  nchi na serikali walikubaliana kwamba wajibu wa kwanza wa kuwalinda raia  dhidi ya udhalimu wa aina yoyote ile ni wa serikali yenyewe husika.

Kupitia dhana hiyo ya R2P  viongozi hao walikubaliana pia kwamba ikiwa itadhihirika kuwa serikali ya nchi husika inashindwa kuwalinda raia wake kwa sababu zozote zile basi  jumuiya ya kimataifa inapashwa  kuchukua maamuzi ya kuwalinda raia hao.

Akichangia majadiliano hayo  ambayo yaliyofunguliwa na Katibu Mkuu   Ban Ki moon, Katika   Balozi Manongi, ameeleza kwamba,  dhana ya  kuwalinda raia inapashwa pia kuhusisha tatizo la wakimbizi wanaokimbia nchi zao kwa sababu mbalimbali na kwenda kutafuta usalama katika mataifa mengine.

Akasema ,  Tanzania ambayo kwa miaka mingi imekuwa  ikiwapokea na kuwahifadhi wakimbizi  kutoka mataifa mbalimbali,  kwa uzoefu wake  inatambua dhahiri kuwa ushirikiano wa kimataifa ni muhimu  sana na kwamba Jumuiya ya kimataifa inatakiwa kuuboresha na kuimarisha ushirikiano huo.

 “Tatizo  linaloendelea hivi sasa la  wimbi kubwa la wakimbizi wanaokimbilia  Ulaya wakitokea Syria, Libya na  kwingineko,  ni changamoto yetu sote,  ni changamotoya kimataifa, wakimbizi hawa  na wengineo wanapashwa kulindwa na kusaidiwa kwa mujibu  wa sheria za kimataifa zikiwamo sheria za haki za binadamu  ”.

 Akasema  Balozi Manongi.
“ Tanzania   kama nchi ambayo kwa miaka mingi imekuwa  ikiwapokea na kuwahifadhi wakimbizi,  inatambua kwamba  ushirikiano wa kimataifa ni muhimu katika kuwasaidia wakimbizi.  Ni   Muhimu basi  tuimarisha na kuboresha misingi ya  kusaidiana  katika kulibeba jukumu hili” akasema Balozi Manongi
Akizungumzia  Zaidi kuhusu dhana ya  wajibu wa kuwalinda raia,  dhana ambayo  tafsiri yake bado  haijapokelewa vema  miongoni mwa nchi wanachama   Balozi amesema. Tanzania inaamini kwamba kanuni za sheria za kimataifa zikiwamo zile za  uhusiano na ushirikiano baina ya  nchi marafiki ni muhimu  katika  kuielewa,  kutafsiri  na utekelezaji wa dhana ya wajibu wa kuwalinda raia kutoka na ukweli kwamba  ni dhana ambayo  haijjitegemei.

Aidha   Mwakilishi huyo wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa,  amebainisha kuwa,  ingawa wajibu wa kwanza wa utekelezaji wa wajibu wa kuwalinda raia  ni wa Nchi au Serikali husika,  lakini  nchi  hiyo inaposhindwa kutimiza wajibu wake huo,  basi Jumuiya ya Kimataifa inapashwa kusaidia kwa kuiwezesha nchi hiyo kutekeleza wajibu huo.

Awali Akifungua majadiliano hayo Katibu Mkuu, Ban Ki Moon,  asema,   ni jambo la kusitikisha sana kwamba  miaka kumi tangu kuasisiwa   kwa dhana hiyo ya R2P   bado watu wengi wakiwamo watoto  wameendelea kupoteza maisha  kutokana  na sababu mbalimbali zikiwamo za vita na migogoro.

“ Ninasikitiza kueleza  kwamba miaka  kumi  tangu kuanzishwa kwa dhana  hii, dunia imeendelea kushuhudia  matukio ya watu  kupotezesha maisha yao kwasababu tumeshindwa kuwalinda. Tunaendelea kushuhudia watu wakipoteza maisha huko Sudan ya Kusini, Sudan katika jimbo la Darfur, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Libya, Syria, Yemen, Mali,  Jamhuri ya Afrika ya Kati  na kwiengineko”.akaeleza Ban Ki Moon. 

Na kwa sababu hiyo Katibu  Mkuu amependekeza  mambo  kadhaa ambayo  anaamini yatasaidia  kuongeza kasi ya utekelezaji wa dhana hii.
Baadhi ya Mambo  hayo ni,    nchi wanachama na hasa Baraza Kuu la Usalama, kuwa tayari  kwa kuweka mazingira ya kisiasa  ya  kuzuia na  kuitikia pale  inapojidhirisha  kuwapo kwa dalili za kutokea kwa uhalifu, utoaji wa tahadhari na kuchukua hatua. 

Wazungumzaji wengine katika   mkutano huo  wamelinyoshea  kidole   Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa na hasa katika matumizi ya kura ya Veto  yanayofanywa na wajumbe wa kudumu wa baraza hilo.

Baadhi ya wachangiaji wameeleza kwamba ili kanuni ya wajibu wa kuwalinda raia  iweze kutekelezwa kwa haraka na kwa wakati, wajumbe wa  watano wa kudumu wa  Baraza Kuu la Usalama, wanapashwa  kuonyesha utashi wa kisiasa na kuacha kutumia kura hiyo  kwa maslahi binafsi.

Wajumbe wengine , licha ya kuelezea  nchi zao kutoridhishwa  kwa  tafsiri  ya dhana  ya wajibu wa  kuwallinda raia lakini pia wamesema  hawakubaliani na matumzi ya nguvu kuingilia nchi nyingine kwa  na hata kuwaondoa   madarakani viongozi kwa  kisingizio    utekelezaji wa dhana ya wajibu wa kuwalinda raia. 

 Wajumbe wengine wameeleza  wazi wazi kupinga  kwao  hoja ya  kutaka  kuingizwa kwa  dhana hiyo ya R2P  katika ajenda  za Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.  Sababu  zikiwa ni pamoja na kuwa  dhana hiyo bado inautata  na inahitaji kuendelea  kujadiliwa  miongoni mwa nchi wanachama.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad