BENKI ya Exim Tanzania imesaini makubalino ya mkopo wenye thamani ya dola za kimarekani milioni 20 (takribani 42bn/-) na kampuni binafsi ya ukopeshaji ya nchini Ujerumani, Deutsche Investitions und Entwicklungsgesellschaft MBH (DEG), lengo likiwa ni kusaidia kuinua sekta ya biashara ndogo hapa nchini(SMEs).
Kwa mujibu wa Afisa Mkuu wa Fedha wa Benki ya hiyo, Bw. Selemani Ponda fedha hizo zilizo katika mfumo wa mkopo mkubwa, zitatolewa kwa awamu mbili kwa kuzingatia maendeleo ya ukuaji katika kusaidia sekta hiyo.
“Mkopo huu mkubwa unakuja wakati muafaka ambapo uchumi unazidi kuimarika huku tukishuhudia mapinduzi makubwa ya kibiashara. Biashara ndogo zinafanya jitihada za kila namna viingie katika kundi la kati.
Huu ni wakati sahihi kwa benki yetu kuongeza nguvu katika sekta hii,” alisema Bw. Ponda katika taarifa aliyoitoa kwa vyombo vya habari jijini Dar es Salaam mwishoni mwa juma lilipita.
Alisema kuwa benki hiyo imeendelea kuwekeza katika kufanya tafiti na kuelewa mahitaji ya wafanyabiashara wadogo hapa nchini jambo lililoiwezesha benki hiyo kubuni bidhaa na huduma zinazokidhi mahitaji ya viwanda hivyo.
Kwa mujibu wa kumbukumbu za benki hiyo hadi kufikia sasa imekopesha jumla ya Tsh. 582bn/- huku 291bn/- kati ya kiasi hicho zikiwa zimetolewa kwa sekta ya biashara ndogo na zile za kati.
Bw. Ponda alisema kuwa benki hiyo inaona fursa ya kipekee kutoa mikopo katika sekta hiyo muhimu wakati ambapo kuna maendeleo makubwa ya kiuchumi nchini.
Alibainisha kuwa benki hiyo, kwa zaidi ya muongo mmoja, imeendelea kuimarisha uhusiano mzuri na taasisi za kimataifa za kufadhili maendeleo ikiwa ni pamoja na IFC, PROPARCO, NORFUND na FMO.
“Kwa kusaini makubaliano haya na DEG, inadhihirisha jinsi ambavyo taasisi hizi za kimataifa za kufadhili maendeleo zina imani na benki yetu,” alisema kwa kujiamini.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa taasisi za fedha barani Afrika na Amerika Kusini kutoka kampuni hiyo ya DEG Bi. Gudrun Busch alisema mkopo huo utasaidia kuongeza nguvu katika kuleta maendeleo kwenye sekta ya biashara ndogo na za kati kote nchini na utasaidia kutatua changamoto mbalimbali katika ukuaji wa uchumi,
“Kwa kufanya hivi, tutakuwa tumechangia katika kuimarisha sekta ya uchumi nchini Tanzania na kutengeneza na kulinda ajira,’’ aliongeza.
No comments:
Post a Comment