JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


TANZANIA YACHAGULIWA MRATIBU AJENDA YA CLIMATE MOBILITY

Share This

 

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi akihutubia Mkutano kuhusu Uhamaji unaosababishwa na Mabadiliko ya Tabianchi (Global Climate Mobility Forum) uliofanyika jijini Berlin, Ujerumani Juni 18, 2026.
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi (kulia) akiwa na viongozi mbalimbali wakati akishiriki Mkutano kuhusu Uhamaji unaosababishwa na Mabadiliko ya Tabianchi (Global Climate Mobility Forum) uliofanyika jijini Berlin, Ujerumani Juni 18, 2026.



Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imechaguliwa kuwa Mratibu wa Nchi za Afrika katika Ajenda ya Uhamaji unaosababishwa na Mabadiliko ya Tabianchi (Climate Mobility).


Hayo yamejiri wakati wa Mkutano kuhusu Uhamaji unaosababishwa na Mabadiliko ya Tabianchi (Global Climate Mobility Forum) uliofanyika jijini Berlin, Ujerumani Juni 18, 2026.


Akihutubia mkutano huo uliokutanisha zaidi ya nchi 51 duniani, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi ameelezea mikakati ya Tanzania katika kuhakikisha sekta ya hifadhi ya mazingira inakuwa endelevu ikiwemo kurejesha misitu na vyanzo vya maji vilivyoharibika.


Alisema nchi imejizatiti katika kuhamasisha kilimo kinachozingatia hali ya hewa ili kuboresha usalama wa chakula na katika maeneo ya wafugaji, jitihada zinaendelea za kuboresha upatikanaji wa maji, huduma za mifugo na usimamizi endelevu wa nyanda za malisho ili kupunguza uwezekano wa ukame na uhaba wa rasilimali. 


Dkt. Muyungi alisema juhudi hizo za Serikali zinaongozwa zaidi na matarajio ya Dira ya Taifa 2050, inayolenga kuigeuza Tanzania kuwa taifa shirikishi, lenye ustawi, uthabiti na endelevu ambayo inasisitiza jamii zinazostahimili uthabiti, ukuaji wa miji endelevu, kilimo cha kisasa, utunzaji wa mazingira, kujiandaa kwa majanga na fursa kwa vijana na watu walio katika mazingira hatarishi.


“Dira inatambua mabadiliko ya tabianchi kama changamoto kubwa ya maendeleo na inaweka ustahimilivu katikati ya mipango ya kitaifa. Nguzo zake za mabadiliko ya kiuchumi na ushindani, maendeleo ya binadamu na ustawi wa jamii, uendelevu wa mazingira na ustahimilivu wa hali ya hewa, utawala bora na ufanisi wa kitaasisi na uvumbuzi na maendeleo yanayoendeshwa na maarifa hutoa mfumo thabiti wa kushughulikia uhamaji wa hali ya hewa kama sehemu ya maendeleo mapana ya kuhimili hali ya hewa,” alisema.


Aidha, Dkt. Muyungi alieleza kuwa nchi inakabiliwa na changamoto za kupanda kwa kina cha bahari, ukame wa mara kwa mara, mafuriko, uharibifu wa mazingira ambazo zinaaathiri maisha, mifumo ya makazi na maamuzi ya uhamaji wa binadamu hususan wakulima, wafugaji, wanawake na vijana. 


Sanjari na hilo, alisema takriban asilimia 65 hadi 70 ya Watanzania wanategemea sekta zinazoathiriwa na hali ya hewa, hasa kilimo cha kutegemea mvua, mabadiliko ya tabianchi yanahatarisha maisha, usalama wa chakula na maendeleo endelevu.


Hivyo, Dkt.  Muyungi alionesha dhamira ya Tanzania ya kufanya kazi na washirika wote ili kuhakikisha uhamaji wa hali ya hewa unakuwa njia ya ustahimilivu, utu, fursa, na maendeleo endelevu kwa kizazi cha sasa na kijacho.



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad