JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


SUA yaanza Maandalizi ya utafiti wa Mpunga Himilivu kwa mabadiliko ya tabianchi na rafiki kwa mazingira Africa.

Share This

 Na: Calvin Gwabara – Morogoro Tanzania.

Mradi wa Mpunga Himilivu kwa mabadiliko ya Tabianchi na Rafiki kwa Mazingira Barani Afrika (Climate-resilient and Eco-friendly Rice for Africa) (CERA) umechukua hatua muhimu katika kuboresha kilimo cha mpunga kwa kuendesha mafunzo maalum kwa wakusanyaji takwimu katika utafiti unaotarajia kufanyika kwenye Mikoa ya Morogoro, Shinyanga na Songwe nchini Tanzania.

Mtafiti Mkuu wa mradi Prof. Suzana Nchimbi Msolla akizungumza na watafiti hao kabla ya kuanza zoezi hilo.

Mafunzo hayo yamewaleta pamoja washiriki ambao watakuwa mstari wa mbele katika ukusanyaji wa taarifa kutoka kwa wakulima, hatua inayotarajiwa kusaidia kufanya maamuzi sahihi ya kisayansi kwenye utekelezaji wa mradi huo wa utafiti.

Akizungumza na watafiti hao wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mtafiti Mkuu wa mradi Prof. Suzana Nchimbi Msolla alitumia nafasi hiyo kueleza kwa kina kuhusu mradi wa CERA, akieleza malengo, muda wake pamoja na matarajio yake hasa katika  kuimarisha usalama wa chakula nchini.

Prof. Msolla ameeleza kuwa mradi huo unalenga kuzalisha mbegu za mpunga zinazostahimili ukame pamoja na kuhamasisha matumizi ya mbinu rafiki kwa mazingira ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi yanayoleta athari kubwa katika uzalishaji wa mazao hasa zao la mpunga nchini Tanzania.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa wa watafiti hao kwenda kuzingatia usawa wa kijinsia kwa kueleza kuwa mradi unalenga kuwafikia zaidi wakulima wanawake katika maeneo yenye ukame ili kuhakikisha wanufaika wote wanashirikishwa.

Mtafiti huyo pia alizungumzia suala la kujenga uwezo kwa taasisi za ndani kwa kutoa mafunzo kwa watafiti na kuboresha miundombinu ya utafiti wa kilimo.

“Ubora wa takwimu mtakazokusanya ndio utakaoamua mafanikio ya mradi huu na utekelezaji wake hivyo nisihi kutumia utaalamu mlionao na huu mtakaopewa kwenye mafunzo haya kuhakikisha mnapata taarifa sahihi kutoka kwa wakulima,” alisisitiza Prof. Msolla.

Kwa upande wake Mtafiti Mkuu Msaidizi wa mradi huo Dkt. Emanuel Malisa, ambaye aliwasilisha mada kuhusu wajibu, maadili na mwenendo wa wakusanyaji takwimu katika kazi za utafiti amesema wakusanyaji takwimu wanapaswa kuwa waaminifu, wasiwe na upendeleo, walinde siri za washiriki, na wahakikishe wanapata ridhaa ya washiriki kabla ya kuanza mahojiano.

Dkt. Malisa aliongeza kuwa wakusanyaji takwimu hao wanawakilisha mradi mbele ya jamii, hivyo wanapaswa kuzingatia heshima na weledi wa hali ya juu katika kazi zao kwenye kila eneo mabalo watapita kwakuwa tamaduni na mila za maeneo zinatofautiana hivyo wahakikishe wanazingatia mambo hayo ili waweze kupata ushirikiano kwa wakulima na jamii watakayoikuta.

Mafunzo hayo pia yalijumuisha mbinu za kufanya mahojiano, matumizi ya teknolojia ya ukusanyaji takwimu kama KoboToolbox, pamoja na namna ya kukabiliana na changamoto za washiriki kutokutoa taarifa.

Washiriki walipata fursa ya kufanya mazoezi kwa vitendo kupitia uigaji wa hali halisi ya kazi (simulation), hatua iliyowawezesha kujiandaa vizuri kabla ya kwenda kukusanya takwimu halisi kwa wakulima.

Matokeo ya Utafiti ya mradi wa CERA yanatarajiwa kutoa mchango mkubwa katika kuongeza uzalishaji wa mpunga, kuimarisha ustahimilivu wa kilimo dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, na kuboresha usalama wa chakula nchini Tanzania na barani Afrika kwa ujumla.

MATUKIO KATIKA PICHA WAKATI WA MAFUNZO HAYO.









No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad