JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


MKUMBI Yaendelea Kuboresha Mazingira ya Biashara Nchini

Share This

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi akizungumza leo Machi 27, 2026 jijini Dar es Salaam katika Mkutano wa Uhakiki wa Rasimu ya Mpango wa Pili wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI II).
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo, akizungumza leo Machi 27, 2026 jijini Dar es Salaam katika Mkutano wa Uhakiki wa Rasimu ya Mpango wa Pili wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI II).


Na Mwandishi Wetu
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI) umeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji na biashara nchini, hatua inayochochea ukuaji wa uchumi na kuvutia wawekezaji wa ndani na nje.

Dk. Mwinyi ameyasema hayo Machi 27, 2026 jijini Dar es Salaam wakati akizungumza katika Mkutano wa Uhakiki wa Rasimu ya Mpango wa Pili wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI II), ambapo alieleza kuwa mpango huo umewezesha sekta mbalimbali kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi katika kuweka mazingira rafiki ya biashara.

Amesema kupitia maboresho hayo, Serikali imeendelea kuweka misingi imara ya kuvutia uwekezaji huku ikilenga kufikia malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 inayokusudia kuifikisha Tanzania kwenye uchumi wa kipato cha juu.

Kwa mujibu wa Dk. Mwinyi, dira hiyo inalenga kufikia uchumi wenye thamani ya dola za Marekani trilioni moja pamoja na kipato cha wastani wa dola 7,000 kwa kila Mtanzania ifikapo mwaka 2050.

Amesisitiza kuwa ili kufikia malengo hayo, nchi inalazimika kuhakikisha ukuaji wa Pato la Taifa unafikia angalau asilimia 10 kwa mwaka kuanzia 2026 hadi 2050, jambo litakalowezekana kupitia uwekezaji mkubwa katika sekta za uzalishaji, viwanda, kilimo cha kisasa, uchumi wa buluu, nishati na TEHAMA.

“Ni wazi kuwa Serikali pekee haiwezi kufanikisha malengo haya, hivyo ushiriki wa sekta binafsi ni muhimu sana katika kuongeza uzalishaji, ajira na mapato ya taifa,” alisema.

Aidha, amebainisha kuwa takwimu zinaonesha mafanikio ya maboresho ya mazingira ya biashara, akitolea mfano mwaka 2024 ambapo miradi 901 ya uwekezaji yenye thamani ya dola bilioni 9.3 ilisajiliwa na kuzalisha ajira zaidi ya 212,000.

Ameongeza kuwa katika kipindi cha miaka miwili ya 2024 hadi 2025, miradi 1,828 yenye thamani ya dola bilioni 20.3 ilisajiliwa nchini, hatua inayodhihirisha kuimarika kwa mazingira ya uwekezaji.

Dk. Mwinyi amesema Serikali pia imeendelea kuwekeza katika miundombinu ya kimkakati ikiwemo reli ya kisasa, bandari, barabara, nishati na TEHAMA ili kupunguza gharama za uzalishaji na kuongeza ushindani wa uchumi.


Amesema kupitia MKUMBI, Serikali imefanya mapitio ya sheria zaidi ya 94 na kuondoa au kupunguza zaidi ya tozo na ada 628 zilizokuwa kikwazo kwa wafanyabiashara, hatua iliyosaidia kupunguza urasimu na kuongeza uwazi katika utoaji wa huduma.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo, amesema mafanikio ya kuboresha mazingira ya biashara yatategemea pia mabadiliko ya mitazamo kwa watendaji wa serikali wanaosimamia utekelezaji wa sera na sheria.

Amesema rasimu ya MKUMBI II imebainisha changamoto 59 zinazokwamisha biashara Tanzania Bara na Zanzibar na kupendekeza maeneo 11 ya mageuzi yenye hatua 246 za utekelezaji ili kuboresha zaidi mazingira ya biashara.

Naye Waziri wa Kazi na Uwekezaji Zanzibar, Shariff Ali Shariff, amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeanza kufanya mapitio ya Sheria ya Uwekezaji ya mwaka 2003 pamoja na kuanzisha mifumo ya kidijitali ili kurahisisha huduma kwa wawekezaji wa ndani na nje.

Aidha, baadhi ya wafanyabiashara waliohudhuria mkutano huo walisisitiza umuhimu wa kuondoa vikwazo vinavyokwamisha biashara katika ngazi za halmashauri pamoja na kuhakikisha sekta binafsi inashirikishwa kikamilifu katika utekelezaji wa mpango huo.

Mkutano huo ulilenga kukusanya maoni ya wadau mbalimbali kabla ya kupitishwa kwa rasimu ya mwisho ya MKUMBI II, ambayo inatarajiwa kuwa chombo muhimu katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji na kukuza uchumi wa Tanzania.



Matukio mbalimbali katika picha.




Picha za Pamaoja.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad