JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


TAASISI WEZESHI ZIWEKE MAZINGIRA RAFIKI KWA WAFANYABIASHARA, KUINUA SEKTA YA BIASHARA -KUNENGE

Share This

 



Mwamvua Mwinyi,PwaniOktoba 3,2024
MKUU wa mkoa wa Pwani, alhaj Abubakar Kunenge ameziagiza Taasisi Wezeshi, kuwa na Ushirikiano wa karibu na kuweka mazingira rafiki kwa wafanyabiashara wadogo ili kuboresha sekta ya Biashara na Uwekezaji.

Aidha amezitaka Taasisi hizo zisigeuke kero kwa wafanyabiashara hao badala yake ziwashirikishe kwa kuwasikiliza na kuwapa elimu ili kupunguza changamoto zao zinazowakabili.

Kunenge aliyasema hayo ,katika kikao Cha majadiliano Kati ya Sekta Binafsi(PPD) na Serikali kilichofanyika katika Ofisi za Mkoa wa Pwani.

Alisema, "Ni muhimu kufanya mikutano mikubwa inayowajumuisha wafanyabiashara wadogo. Tunapaswa kujitathmini na kuona wapi tunakosea ili kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji."

Aidha, Kunenge aliongeza kuwa ni muhimu kwa wafanyabiashara kusikilizwa na kupata ushauri wa kitaalamu ili kutoa maoni yao kuhusu namna ya kuboresha sekta hiyo.

"Tuwasikilize na tuwape nafasi ya kueleza changamoto zao ili kuweka mikakati bora ya kuwasaidia, badala ya kuwakamua kwa kuwalipisha faini kubwa zisizo na msingi," anaeleza.

Mwenyekiti wa TCCIA Mkoa wa Pwani, Saidi Mfinanga, alieleza kuwa wafanyabiashara wanakabiliwa na faini kubwa, ambazo kwa baadhi ya wafanyabiashara wakubwa zinafikia hadi milioni 20, hali inayosababisha biashara nyingi kufa.

Alisema kodi na tozo hazipaswi kuwa adhabu bali ziwe rafiki kwa wafanyabiashara ili waendelee kukuza mitaji yao.

Abdallah Ndauka, Mwenyekiti wa Wafanyabiashara Mkoa wa Pwani, alisisitiza kuwa wafanyabiashara wanapaswa kushirikishwa katika maamuzi muhimu ili kuhakikisha sekta ya biashara inajengwa badala ya kuangamizwa.

Philemone Maliga, Mwenyekiti wa Wamachinga Pwani, aliomba serikali kusaidia wafanyabiashara wadogo kwa kuanzisha ofisi ya Machinga katika mkoa, Hii itawasaidia kurahisisha shughuli zao na kuongeza tija katika biashara.

Yusta Kaunda kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani aliwasihi wafanyabiashara kutumia mashine za kielektroniki kutoa risiti halali kwa wateja, hatua ambayo itasaidia kudhibiti upotevu wa mapato ya serikali.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad