JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


SERIKALI: KILA HALMASHAURI KUWA NA MSITU WA ASILI KUTUNZA MAZINGIRA

Share This

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (kulia) akiweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa madarasa katika Shule ya Sekondari Bamba Kilifi katika Wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga. Kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt. Batilida Burian.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji akifafanua jambo mara baada ya kuzindua Shule ya Sekondari Kiomoni iliyopo Kata ya Mzizima Halmashaurii ya Jiji la Tanga mkoani Tanga jana Oktoba 23, 2024.

Na Mwandishi Wetu, TANGA
SERIKALI imesema inaandaa mpango wa kwa kila Halmashauri nchini kuwa na misitu ya asili ili kuimarisha mkakati wa usimamizi wa biashara ya kaboni na uhifadhi wa mazingira.

Hayo yamesemwa Oktoba 23, 2024 na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Ashatu Kijaji wakati wa ziara yake Mkoani mkoani Tanga kwa ajili ya kukagua, kufungua na kuweka mawe ya msingi katika miradi ya maendeleo.

Mhe. Dkt. Kijaji ameeleza kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha kila halmashauri nchini inaingia katika biashara ya kaboni kupitia upandaji wa miti ambapo pamoja na uhifadhi wa mazingira, miti pia ni fursa ya kibiashara inayowezesha jamii kujiongezea kipato kwa wananchi na jamii kwa ujumla.

Dkt. Kijaji ameongeza kuwa mpango huo mbali na ushirikishaji wa Halmashauri pia utawalenga wananchi wanaomiliki maeneo makubwa ya ardhi wenye uwezo wa kutumia maeneo yenye ukubwa wa ekari tano hadi 10 kwa ajili ya kupanda miti kibiashara.

“Pamoja na fursa ya biashara, kupitia upandaji miti kutasaidia kupunguza athari za mabadiliko ya tabia nchi ambapo yanasababisha mabadiliko ya hali ya hewa ikiwemo ongezeko la joto na mvua zisizo na mpangilio” amesema Dkt. Kijaji

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian amesema Ofisi yake imekuwa ikiendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu athari za uharibifu wa mazingira ikiwemo uchomaji ovyo wa misitu na kuwahimiza kupanda miti kwa ajili ya uhifadhi na utunzaji wa mazingira.

Ameongeza Mkoa huo una zaidi ya hekta 700,000 za misitu zenye mashamba matatu ya miti, ambapo katika kuendelea kutunza maeneo hayo ofisi yake kwa kushirikiana na mamlaka na idara mbalimbali za serikali imekuwa ikiwahimiza wananchi kutunza maeneo hayo na kuacha kuuingiza mifugo ndani ya hifadhi hizo.

Amefafanua wananchi wamekuwa na mwamko mkubwa katika kilimo cha mikoko ambacho kinasaidia katika utunzaji wa mazingira ya bahari kwani wakati wa mmomonyoko wa udongo miti hiyo inasaidia kusitokee uharibifu wa mazingira.

Mhe. Dkt. Kijaji yupo katika ziara ya kikazi ya siku tatu Mkoani Tanga iliyoanza tarehe 23 Oktoba kwa ajili ya kukagua kwa ajili ya kukagua, kufungua na kuweka mawe ya msingi katika miradi ya maendeleo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad