JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


TBA WATOA TUZO KWA WALIOFANYA VIZURI KWA 2023/2024 WALIA NA VAT KWENYE MKATE

Share This

 Mshindi wa Kitengo cha Mwanamke mwenye uzalishaji mkubwa ni Salama Mpanga, akikabiziwa tuzo na Preagi kutoka PSSB wakati wa utoaji wa tuzo kwa Waokaji waliofanya vizuri kwa mwaka 2024, tuzo hizo zimefanyika katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar Es Salaam Agosti 27,2024.

Waziri wa Mambo ya Ndani, Daniel Sillo akizungumza wakati wa utoaji wa tuzo kwa Waokaji waliofanya vizuri kwa mwaka 2024, tuzo hizo zimefanyika katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar Es Salaam Agosti 27,2024.


SERIKALI tunachukua suala la Kodi ya ongezeko la thamani (VAT) katika tasnia ya Uokaji nchini kwa uzito kwani tunaelewa gharama inapokuwa kubwa hupelekea wazalishaji wasio waaminifu kutumia malighafi hafifu zinazopelekea bidhaa zisizozingatia kanuni za ubora na hivyo kupelekea watumiaji kupata maradhi kutokana na vyakula visivyo na ubora.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Daniel Sillo wakati wa utoaji wa tuzo kwa Waokaji waliofanya vizuri kwa mwaka 2024, tuzo hizo zimefanyika katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar Es Salaam Agosti 27,2024. Amesema kuwa tayari Rais Dkt. Samia alishaunda tume maalumu ya Rais ya kutathmini na kuishauri serikali kuhusu masuala ya kodi hiyo ni kutokana na kero mbalimbali za wafanyabiashara ikiwamo Waokaji.

Sillo, ameahidi kupeleka maoni ya sekta hiyo ya uokaji katika Tume ya Rais ya masuala ya kodi ili yaweze kutatuliwa ipasavyo.

"Tasnia ya Uokaji ni muhimu kwa ustawi na maendeleo ya uchumi wetu kwani si tuu kwamba inachochea kujiajiri na kipato cha jamii lakini inawezesha watanzania kula chakula bora salama na cha uhakika kwa hiyo mafanikio ya tasnia hii ni ya jamii kwa ujumla." Amesema

Pia ameeleza kuwa nia ya serikali ni kuhakikisha inaweka mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara hasa wa Waokaji ambao wameajiri watanzania wengi kwa niaba ya serikali.

Amesema kuwa tasnia ya Uokaji hapa nchini ina nafasi kubwa ya kukua na kuchangia zaidi katika katika uchumi wa taifa.

"Ni jukumu letu sote kuhakikisha kuwa ukuaji huo unakuwa na manufaa kwa wazalishaji, walaji na taifa kwa ujumla." Ameeleza

Pia amesisitiza vyama vyote vilivyosajiliwa na Wizara ya Mambo ya ndani ya nchi kuhakikisha wanawasilisha taarifa zao mara kwa mara.

Kwa upande wa Mwenyekiti wa Chama Cha Waokaji wa Mikate na keki Tanzania(TBA), Fransisca Lyimo ameiomba Serikali kuwaondolea kodi ya Ongezeko la thamani (VAT) katika mkate.

"Tunaiomba Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan VAT, ikiwepo kwenye Mkate ni Changamoto ambayo inaifanya sekta ya Uokaji Tanzania isikue."

Amesema kuwa tasnia hiyo ambayo inaingia kwenye mahitaji muhimu ya binadamu katika kipengele cha Chakula VAT haiwezi kuongeza gharama ya mkate kwani VAT imekuwa kikwazo kikubwa katika tasnia hiyo.

"Ukiangalia nchi za Afrika Mashariki bei ya mkate ni ndogo ukilinganisha na Tanzania, Kenya wanazalisha mikate kwa uwingi lakini Tanzania muokaji anashindwa kuzalisha kwasababu ya kodi hiyo." Amesema Fransisca

Akiizungumzia sekta hiyo yenye wanachama 305 ambayo unaweza kuanza kuifanya kwa mtaji mdogo Fransisca amesema kuwa tozo na kodi nyingi nazo ni kikwazo cha kukua kwa sekta hiyo na anatamani kuona sekta hiyo ikuwe na iweze kulisha jamii kubwa ya Watanzania.

Mliki wa Dexterous Sweet and Healthy Treats, Celine Ngahugha amesema kuwa maendeleo ya tasnia hiyo inawapa hamasa ya kuendelea kuoka kwani kwa sasa keki sio chakula cha anasa.

Akitolea mfano Celine amesema "Keki ya harusi ni lazima hata kama kukiwa na ndafu lakini keki lazima iwepo, ila wakati ule tunaanza 'baking' kuoka keki ilikuwa si lazima."

Katika Chakula cha jioni hicho cha TBA kiliwakusanya wadau mbalimbali na wanachama kwaajili ya kujadili changamoto, nini kifanyike na kutambua mchango wa waliofanya vizuri na kuwapa tuzo katika vitengo mbalimbali ambavyo wameshinda tuzo 15 kulingana na Vitengo ikiwa Mshindi wa jumla ni Bakheresa, mshindi wa kwanza tuzo ilikwenda kwa Salma Mpanga, wapili ni Fransisca Lyimo, akifuatia Atul Sheith, Super Loaf na mshindi wa tano ni Sun Kist Baker ikifuatiwa na washindi wengine 10.
Mshindi wa Kitengo cha Mwanamke mwenye uzalishaji mkubwa ni Salama Mpanga akizungumza na waandishi wa habari wakati wa utoaji wa tuzo kwa Waokaji waliofanya vizuri kwa mwaka 2024, tuzo hizo zimefanyika katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar Es Salaam Agosti 27,2024.
Mliki wa Dexterous Sweet and Healthy Treats, Celine Ngahugha akizungumza na waandishi wa habari wakati wa utoaji wa tuzo kwa Waokaji waliofanya vizuri kwa mwaka 2024, tuzo hizo zimefanyika katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar Es Salaam Agosti 27,2024.










Matukio mbalimbali.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad