JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


WAZIRI WA NISHATI ATAKA MITAMBO YOTE YA MADINI ITUMIE UMEME

Share This

Na Veronica Simba – Mara
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amesema Serikali kupitia Wizara anayoisimamia, imejipanga kuhakikisha wawekezaji wote katika sekta ya madini wanatumia umeme katika shughuli zao ili wazalishe kwa tija itakayowawezesha kulipa kodi stahiki kwa Taifa na hivyo kukuza uchumi wa nchi. 

Alitoa kauli hiyo, Septemba 18, 2018 mkoani Mara, wakati akizungumza na Mkuu wa Mkoa Adam Malima ofisini kwake, kabla ya kuanza ziara ya kazi katika Mkoa huo, kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme.

“Tunataka migodi izalishe kwa tija ili kusudi ilipe kodi, ushuru na tozo zote stahiki kwa Serikali hivyo kukuza uchumi wa nchi yetu.”

Kauli hiyo ya Waziri Kalemani, aliitoa kufuatia ombi la Mkuu wa Mkoa kuhusu kuupatia nishati ya umeme Mgodi wa Dhahabu wa Nyamongo uliopo mkoani humo; ambapo Waziri Kalemani alimhakikishia kuwa Wizara yake inakamilisha taratibu za kuunganisha umeme katika Mgodi huo ndani ya muda mfupi, baada ya mwekezaji huyo kukamilisha malipo.

Alisema kuwa, tayari alishamwagiza Meneja wa TANESCO wa Mkoa wa Mara, Mhandisi Emmanuel Kachewa kuhakikisha Mgodi huo unaunganishiwa umeme kabla ya mwezi huu kuisha.

Waziri Kalemani alisema kuwa kwa muda mrefu, wengi wa wawekezaji katika sekta ya madini wamekuwa wakitumia mafuta katika kuendesha mitambo hiyo hivyo kulalamika kwamba wanatumia gharama kubwa inayowasababishia hasara katika uzalishaji hivyo kushindwa kulipa kodi stahiki za Serikali kadri ipasavyo.

Alifafanua kuwa, ni kwa sababu hiyo, Serikali imedhamiria na ilikwishaanza kutekeleza mpango wa kuhakikisha wawekezaji wote wa sekta husika, wakiwemo wakubwa, wa – kati na hata wadogo wanatumia umeme ili kuondoa visingizio vya kuendesha shughuli zao kwa hasara na hivyo kutokulipa kodi ipasavyo.

Katika hatua nyingine, Waziri Kalemani ametoa wito kwa taasisi zote zinazodaiwa na TANESCO, kuendelea kulipa madeni yao ili kuliwezesha shirika hilo la umma kuwahudumia watanzania kwa viwango na ubora.

“TANESCO isipolipwa madeni inayozidai taasisi na hata wateja binafsi, inapata shida kuwahudumia wateja wake ambao ni Watanzania. Kwahiyo, tunahamasisha wote ambao bado hawajalipa Ankara za umeme kuendelea kulipa ili kuipunguzia Serikali mzigo,” alisisitiza.

Katika ziara hiyo, Waziri Kalemani alitembelea maeneo mbalimbali ambapo aliwasha umeme katika vijiji vya Nyakatende, Musoma Vijijini na Bubombi kilichopo Wilaya ya Rorya pamoja na kuzungumza na wananchi. 

Aidha, alitembelea kijiji cha Nyamohonda kilichopo wilayani Tarime, mpakani mwa Tanzania na Kenya na kuwaahidi wananchi kuwa watapata huduma ya umeme hivi karibuni kwani tayari kazi hiyo imekwishaanza kutekelezwa.

Awali, akiwasilisha kwa Waziri taarifa ya utekelezaji wa miradi ya umeme katika eneo lake, Meneja wa TANESCO Mkoa wa Mara, Mhandisi Emmanuel Kachewa alisema kuwa jumla ya vijiji 273 vitapatiwa umeme kupitia Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu, Sehemu ya Kwanza (REA III – Phase 1), ambao umekwishaanza kutekelezwa na unatarajiwa kukamilika ifikapo Juni, 2019.
 Mkuu wa Mkoa wa Mara, Adam Malima (kulia), akimweleza jambo Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani, muda mfupi kabla ya Waziri kuanza ziara yake mkoani humo kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme na kuzungumza na wananchi, Septemba 18, 2019.
 Mwonekano wa nyumba ya mmoja wa wakazi wa Kijiji cha Nyakatende, Wilaya ya Musoma Vijijini, muda mfupi kabla ya Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani kuiwashia umeme ikiwa ni ishara ya uwashaji rasmi wa huduma ya nishati hiyo katika eneo hilo. Tukio hilo lilifanyika 18, 2019.
 Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani akiwasha umeme katika nyumba ya mmoja wa wakazi wa Kijiji cha Nyakatende, Musoma Vijijini, ikiwa ni ishara ya uwashaji rasmi wa nishati hiyo katika eneo hilo. Waziri alikuwa katika ziara ya kazi mkoani humo, Septemba 18, 2018 kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme.
Meneja wa TANESCO Mkoa wa Mara, Mhandisi Emmanuel Kachewa akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi ya umeme mkoani humo, kwa Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani (hayupo pichani), alipowasili katika Mkoa huo kwa ajili ya ziara ya kazi Septemba 18, 2018.
 Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (kulia), akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Bubombi, Wilaya ya Rorya mkoani Mara, muda mfupi kabla ya kuwasha rasmi umeme katika eneo hilo. Hafla hiyo ilifanyika Septemba 18, 2018.
 Sehemu ya umati wa wananchi wa Kijiji cha Nyakatende, Musoma Vijijini wakimsikiliza Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (hayupo pichani), alipokuwa akizungumza nao wakati wa hafla ya uwashaji rasmi umeme katika eneo hilo, Septemba 18, 2018.
Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani, akisalimiana na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Mara, alipowasili katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Septemba 18, 2018 muda mfupi kabla ya kuanza ziara ya kazi mkoani humo kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme.                     

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad