JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


BARAZA KUU LA USALAMA LA UMOJA WA MATAIFA LAIJADILI BURUNDI

Share This
Matthew Rycroft, Mwakilishi wa Kudumu wa Uingereza katika Umoja wa Mataifa na Rais wa Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa,  kwa mwezi  Novemba, akizungumza na waandishi wa habari   hawapo pichani, mara baada ya  Baraza Kuu la Usalama kumaliza kikao chake kilichojadili hali ya  Burundi, kikao ambacho pia kilipitisha azimio ambalo pamoja na mambo mengine linamuunga mkono  Rais wa Uganda  Yoweri Museven ambaye aliteuliwa na  Viongozi  wenzie wa Jumuiya ya Afrika  Mashariki kuwa msimamizi na mwezeshaji wa majadiliano  kati ya pande zinazopinga  nchini Burundi.
 
Na Mwandishi Maalum, New York
BARAZA Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa  limelaani vikali  hali ya  kuendelea kwa matukio ya mauaji, utesaji na vitendo vingine vya  vinavyokiuka haki za binadamu nchini  Burundi.

Pamoja na kukemea hali hiyo,  Baraza Kuu la Usalama  limeeleza  kusudio la kuchukua hatua zaidi kwa nchi hiyo ya  Burundi.  Pamoja na  kumwomba  Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, katika kipindi cha siku  kumi na tano awasilishe mbele ya Baraza hilo taarifa kuhusu  uwepo wa Umoja wa Mataifa nchini  Burundi katika siku za baadaye. 

Jana ( Alhamisi) Baraza hilo  lilikutana katika kikao chake cha 7557   ajenda  ilikuwa ni Burundi ambapo,   Baraza kwa kauli moja  lilipitisha Azimio namba 2248 (2015). Kupitia  Azimio hilo, Baraza limetoa wito kwa  pande zote nchini Burundi kujiepusha na kukataa   fujo ikiwa ni pamoja na kujiepusha na vitendo vyovyote  vinavyoweza kutishia Amani na  utulivu wa taifa hilo.

Vile  Vile Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa ambalo kwa mwezi huu wa  Novemba  Rais wake ni Uingereza limekema vikali kauli za  uchochezi zinazotolewa na baadhi ya  watu ndani na nje ya Burundi, kauli  ambazo kwa mujibu wa Baraza hilo zinalenga katika kushawishi chuki baina ya  makundi ya watu  nchini humo.

 Kufuatia  kauli hizo za uchochezi,  Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa,  limeitaka Serikali ya Burundi kuheshimu, kulinda na kuhakikisha haki za binadamu na  misingi ya uhuru,  kuheshimu utawala wa sheria pamoja na uwajibikaji wa uwazi dhidi ya   fujo na  itoe ushirikiano kwa  Ofisi ya Kamisheni ya Haki za Binadamu.

  Kupitia  Azimio hilo  Baraza Kuu pia  limeitaka serikali ya Burundi kuwawajibisha wale wote watakaopatikana na hatia  ya ukiukwaji ya Sheria ya Kimataifa ya haki za binadamu na unyanyasajji wa haki za binadamu.

Aidha  kupitia  Azimio hilo,  Baraza Kuu la Usalama limetoa wito kwa Serikali ya  Burundi kutoa ushirikiano katika majadiliano yanayoongozwa na Jumuiya ya Afrika  Mashariki  na ambayo yameridhiwa na Umoja wa Afrika na limetaka  kuitishwa haraka majadiliano yatakayokuwa jumuishi yakiwashirikisha wadau mbalimbali kutoka ndani na nje ya Burundi  ili kutafuta muafaka utakaokubaliwa na pande zote.

Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa pia kupitia Azimio hilo limesema linamuunga mkono kwa nguvu zote  mwezeshaji wa  majadiliano hayo  ambaye ni Rais Yower Museveni wa Uganda aliyeteuliwa na  Viongozi wa Jumuiya ya Afrika  Mashariki.

 Katika kusaidia  mchakato wa majadiliano hayo, Baraza Kuu la Usalama  la Umoja wa Mataifa limemkaribisha Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa  kupeleka  timu  ya wataalam ambao kwa kushirikiana  na Serikali, Umoja wa Afrika na wadau wengine watabuni   mbinu  za  kushughulikia matatizo ya kisiasa na kiusalama.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad