JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


MWALIMU NYERERE KATIKA UGA WA USHAIRI

Share This
  RAIS wa awamu ya kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere  alizaliwa mwaka 1922 katika  Wilaya ya Butiama Mkoa wa  Mara, mnamo tarehe 14 Oktoba, 1999, aliaga dunia katika hospitali ya mtakatifu  Thomas  Jijini London  nchini Uingereza.  

Katika uhai wake,  alikuwa ni Mmalenga.   
Aliandika barua ya Kiserikali kwa mtindo wa utenzi, pia alijibiwa barua hiyo  kwa mtindo wa utenzi na Nguli/Karii,  Hayati Saadani Abdul Kandoro aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo mnamo mwaka 1964.

Nukuu ya Hayati Saadani A. Kandoro “Huu ni utenzi ulioandikwa kwa njia ya barua iliyotungwa na Muheshimiwa Mtukufu mwalimu J.K. Nyerere  President wa TANU na Serikali. Aliniletea barua hiyo ili kunizungumza jinsi ya watu wanaopenda kujisaidia katika shughuli za maendeleo na jinsi ya kuwapa moyo dhidi ya adui wa jamii katika shughuli za vijiji”.
 Picha ya Hayati Mw. J.K. Nyerere

                       SHEIKH KANDORO, SIKIA!
1.     Sheria  husaidia,
Kuijenga Tanzania,
Siyo kazi ya sheria,
     Nchi kutuharibia.

2.     Kila nchi ina nia,
Inayoikusudia,
Vile vile ina njia,
   Itakayoipitia.

3.     Tanzania tuna nia,
Ya kujenga ujamia,
Na  njia ya kupitia,
  Ni wote kusaidia.

4.     Kijiji cha turadhia,
Kisima kujipatia,
La magambo limelia,
  Watu wakahudhuria.

5.     Wakakubali kwa nia,
Kisima kujichimbia,
Aliyewakatalia,
   Kukuye wakamlia.

6.     Akenda kushtakia,
Kwa hakimu wa sheria,
Kwamba wamemuonea
    Kuku wake kalmia.

7.     Hakimu akasikia,
Akaita jumuia,
Wakaja akawambia,
    Nyinyi wavunja sheria.

8.     Basi nawahukumia,
Faini shilingi mia,
 Na sabini za fidia,
    Au jela kuingia.

9.     Hakimu wakamwambia,
Itatushinda fidia,
Hata na faini pia,
    Heri jela kuingia.

10.             Wakafungwa kwa sheria,
Na maji wakamwachia,
Mwenye kuku kuumia,
     Pamwe na Hakimu pia.

11.             Huko ni kusaidia,
Adui wa jumuia,
Nasi kazi ya sheria,
    Ila ya maharamia.

12. Kazi hasa ya sheria,
Kusaidia raia,
Sina nia kuwavunjia,
Wanapojisaidia.

“JIBU LA SHEIKH S.A. KANDORO ALIYEKUWA AREA COMMISSIONER BAGAMOYO, KWA SHAIRI LA MHESHIMIWA MWALIMU J.K.NYERERE, RAIS WA JAMHURI YA TANZANIA”
“Huu ni utenzi niliandika kama barua ya kumjibu Mheshimiwa Mtukufu Mwalimu J.K. Nyerere President wa TANU kujibu utenzi wake alioniandikia juu ya wanaoharibu maendeleo ya kijiji katika kazi za jamii”.

Picha ya Hayati sheikh S. A Kandoro

1.     Labeka Mheshimiwa,
Julius msifiwa,
Kambarage muelewa,
    Bwana nakuitikia.

2.     Nakuitikia sheria,
Kwamba inasaidia,
Kuijenga Tanzania,
    Na ni nguzo ya Dunia

3.     Kutoheshimu sheria,
Huleta wingi udhia,
Amani ikapotea,
     Nchi zikaangamia.

4.     Ni msumeno sheria,
Mithali hii natia,
Haitaki kubabia,
    Pendelea liso njia.

5.     La mgambo likilia,
Watu wote hudhuria,
Kisima kujichimbia.
     Hilo lataka sheria.

6.     Kuna wavivu wa nia,
La mgambo likilia,
Nao anajikalia,
   Huendi kuhudhuria.

7.     Mfano huo hatia,
Wengine huufatia,
Na wao hujikalia,
Kazi zetu husinzia.

8.     Kimila nimesikia,
Waweza kumsikia,
Kuku wake kujilia,
Lakini sio sheria.

9.     Kwa kuwa sio sheria,
Mvivu hujishitakia,
Na walao huumia,
Pia hutozwa fidia.

10.            Twazidi kukulilia,
Ifanywe hasa sheria,
By Law kuitia,
Yaweza kusaidia.

11.            Yaweza kusaidia,
Kuku tukijilia,
Pasiwepo hata njia,
Mvivu kukimbilia.

12.            Kuku tumejilia,
Pasiwe na kuponyea,
Hakimu kumuendea,
Kwamba alipwe fidia.


13.            Mkazo twaukazia,
Bila nyuma kurudi,
Twataka kuendelea,
Kuinua Tanzania.

14.            Taifa kuitikia,
Kazi kuzishangilia,
Ndilo tunalolilia,
Ndipo tunakazania.

15.            Ndipo tuna kazania,
Na tena tuna kania,
Kuishangaza dunia,
Lengo letu kutimia.

16.            Bila nguvu kuzitia,
Mkazo wa kisheria,
Unafaa kufatia,
Kazi zitaendelea.

Utii wa Sheria bila kushurutishwa:

Nukuu ya  S .A . Kandoro , Mashairi ya Saadan,
(Jina la Ushairi ; Staharaki kwa tendo ),
  (UK. 162-166)
Mnukuu; Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo;
Idara ya Maendeleo ya Utamaduni; Sehemu ya Lugha.
Hajjati  S . Kitogo na C. Mhongole

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad