Milipuko mikubwa ya mabomu imetokea leo huko Mbagala katika ghala ya silaha ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania, milipuko ambayo imesababisha wasiwasi mkubwa kwa wakazi wa Jiji la Dar na vitongoji vyake.
Habari za awali zinasema kuwa milipuko hiyo siyo jambo la mazoezi bali ni ajali. Hadi hivi sasa idadi taarifa za awali zinasema watu watatu wamekufa na wengine wengi kujeruhiwa na kukimbizwa kwenda hospitali ya Temeke na hospitali nyingine za jirani. Taarifa za awali za kijeshi zilitoa wito kwa wananchi walioko ndani ya usawa wa kilomita 25 kuhama maeneo yao na muda mfupi uliopita Naibu Waziri wa Ulinzi Bw.
Emmanuel Nchimbi amerudia wito huo kupitia ITV na kuwataka watu waliokuwa kwenye majengo marefu kuteremka. Milio na mtikiso wa mabomu hayo umesikika hadi maaeneo ya Msasani upande mwingine wa Jiji la Dar huku maofisi na maeneo ya makazi baina ya pande hizo mbili yakiwa katika hali ya wasiwasi, na watu wakipata na mshtuko.
Kufuatia mlipuko huo Polisi wametoa maelekezo kuwa mtu yeyote akiona kifaa cha chuma ambacho kimeangukia kwenye nyumba yake au eneo lake asijaribu kukihamisha bali kutoa taarifa Polisi kwani kuna mabomu mengine yamerushwa katika mlipuko huo lakini bado hayajlipuka.
Vivyo hivyo, serikali imeahidi kuwahudumia bure wale wote ambao wamejeruhiwa katika mlipuko huo na kusaidia katika kukarabati makazi ya wale ambao nyumba zao zimeharibiwa kufutia mlipuko huo mkubwa. Vyanzo mbalimbali vya habari vinadokeza kuwa wengi wa waliojeruhiwa ni pamoja na watoto wa shule ya Msingi ambayo iko jirani na eneo hilo na wakazi ambao nyumba zao zimelizunguka ghala hilo.
Juhudi za uokoaji na udhibiti wa hali zinaendelea kukiwa na ushirikiano kati ya Jeshi la Wananchi, Polisi na vyombo vingine vya usalama pamoja na vyombo binafsi vya uokoaji kama Ultimate Security. Jiji la Dar ambalo lina wakazi karibu milioni tatu lina kituo kimoja tu cha Uokoaji na haijulikani kama Jeshi la Wananchi wa Tanzania linakituo chake cha Zimamoto kwani katika eneo la Dar na Pwani Jeshi hilo lina kambi mbalimbali, mahospitali pamoja na vikosi vingine mbalimbali.
Kwa upande wa JWTZ, kuna wanajeshi ambao wamekufa kishujaa katika jitihada za kukabiliana na mlipuko huo ili kuzuia mabomu yasidhuru jamii zaidi. Kwa hesabu yoyote leo itakuwa ni siku ya majonzi makubwa kwa Taifa kwani idadi ya waliokufa inaweza kuwa kubwa sana na ya wale waliojeruhiwa kupita hata ukadiriaji wa haraka.
Madhara kwa nyumba na vitu mbalimbali inakadiriwa kupitia mabilioni. Tunaombea hilo halitakuwa hivyo vumbi zima likishatulia. KLHN na wasomaji wake wote tunaungana na serikali kutoa wito kwa wananchi kufuata maagizo yote yanayotolewa na vyombo vya usalama wakati huu na kuhakikisha kuwa wakati kama huu kama kitu kimoja tunaweka tofauti zetu pembeni na kuhakikisha tunasaidiana.
Tusimame pamoja na kuzuia uporoji wowote ambao unaweza kutokea kwenye nyumba za wale walioathirika na tusikubali watu wachache watumie tukio hili kama nafasi ya kufanya uhalifu. Tunatoa taasisi mbalimbali ambazo zinauwezo kuanza mara moja kutoa misaada ya kiutu kusaidia wale wote walioathirika, kujeruhiwa au kupoteza vitu mbalimbali kwani tukio hili japo tutajua zaidi chanzo chake hapo baadaye ni msiba wa taifa letu na kimguse kila mmoja kama tulivyoguswa na mambo ya kipuuza ya zeutamu! Hili ndilo tukio la kutuunganisha Watanzania wote wakati huu na mambo ya nani awajibike au asiwajibike yaje baada ya kuhakikisha kuwa hali imerudishwa katika usalama, waliojeruhiwa wanajulikana na hatua madhubuti zimechukuliwa kuhakikisha usalama wa eneo hilo.
Kutoka hapo, ndipo sauti zetu zipae juu ya jinsi gani tukio hili lingeweza kuzuiliwa kwani wengine tuliandika mambo haya karibu mwaka mzima kwa sababu tunaamini Jiji la Dar limekaa katika hali ya majanga makubwa sana. Na hili yawezekana ni dokezo tu. Tutasema zaidi baadaye. Tunawaombea rehema wale waliopoteza maisha yao, unafuu na uponyi wale waliojeruhiwa na ujasiri na moyo wa kujitoa zaidi kwa wale ambao wanasimama kuhakikisha usalama wa Taifa letu.