JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


Vyama vya michezo nchini vyaaswa Kutoa shukrani.

Share This
Na Eleuteri Mangi-MAELEZO
Vyama vya michezo nchini vimeaswa kuthamini na kutoa shukrani baada ya kumaliza mashindano kwa lengo la kuimarisha ushirikiano pamoja na kuwapa moyo wanamichezo na wadhamini wa mashindano.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu wa Baraza la Michezo Tanzania (BMT) Mohamed Kiganja wakati wa hafla ya kukabidhi zawadi na vyeti kwa washiriki, wadhamini na waandishi wa habari waliofanya vizuri katika kupiga picha na kuandika habari za Mashindano ya Magari yaliyofanyika Julai 8 hadi 10 wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani na kusimamiwa na Taasisi ya Automobile Association Tanzania (AATanzania). 

 “Vyama vingine vya michezo nchini vinapaswa kuiga mfano wa AATanzania wa kutoa shukrani baada ya mashindano, hili ni fundisho kubwa, wanapaswa kuthamini na kutambua msaada wa kufanikisha mashindano yeyote wanayoyaandaa” alisema Kiganja.

Katibu huyo aliongeza kuwa, yanafanyika mashindano ya michezo mbalimbali nchini yakiwa lengo la kuburudisha na kuelimisha jamii, ni wajibu wao kuiga mfano uliouoneshwa na AATanzania wa kutoa shukrani baada ya mashindano.

Naye Rais wa AATanzania Bw. Nizar Javan ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na BMT ambao wamekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha mashindano hayo yaliyofanikiwa kwa ufanisi mkubwa.

Bw. Nizar aliongeza kuwa mashindano hayo yaliisha salama bila ya kutokea ajali yeyote hatua ambayo inaendana na kauli mbiu yao inayosema “Usalama kwanza”.

Kwa upande wa Jeshi la Polisi, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Afisa Mnadhimu Kikosi cha Usalama Barabarani (SACP) Fortunatus Musilimu amewashukuru AATanzania kusimamia, kuandaa na kufanikisha mashindano hayo ambayo yamezingatia usalama wa washiriki wa mashindano na magari yaliyotumika.

Katika kuitangaza Tanzania kupitia mchezo wa magari, Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari (MAELEZO) Zamaradi Kawawa amewasihi waandaaji wa mashindano hayo kuebdelea kuhamasisha wachezaji wa mchezo huo kujitokeza kwa wingi na kushiriki mashindano hayo, hatua ambayo itasaidia kuongeza ushindani na kuitangaza Tanzania Kimataifa kwa kuwa mchezo huo unashirikisha mataifa malimbali.

Waandishi wa habari waliopata vyeti na zawadi kwa kuuhabarisha umma juu ya mashindano hayo ni pamoja na Mohamed Ugassa kutoka gazeti la The Guardian, Jimmy Tara wa ITV, Brown Msyani kutoka gazeti la Citizen, Timzoo Kalugira na Michael Maluwe kutoka Azam Tv, Nasongelya Kilyinga gazeti la Daily News na Miguel Suleyman ambaye ni wandishi wa habari wa kujitegemea.

Pamoja na waandishi hao, wadau waliopewa zawadi kwa kutambua mchango wao katika kufanikisha mashindano hayo ni Jeshi la Polisi, Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Baraza la Michezo Tanzania na Hoteli ya Southern Sun. 

Mashindano hayo ya magari yaliyofanyika nchini yanatambuliwa na Shirikisho la Michezo ya Magari Duniani (FiA) ambayo AATanzania ni mwanachama.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad