JIACHIE

Karibuni Jamvini Wanajamii

Tangaza Hapa

Post Top Ad


TANGA YAANZA MAANDALIZI MRADI WA BOMBA LA MAFUTA

Share This

 Mkurugenzi wa Sheria, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Ibrahim Ngabo, akizungumza na waandishi wa Habari wakati Mkuu wa Mkoa wa Tanga alipotembelea eneo la Chongoleani itakapojengwa gati itakayotumika kupakua mafuta ghafi.
 Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Martine Shigella, akiongea jambo mara baada ya kutembelea eneo la Chongoleani Mkoani Tanga, itakapojengwa Gati itakayotumika kupakua mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda.
 Mkuu wa Mkoa wa Tanga , Martine Shigella ( Wa tano kutoka kulia), katika picha ya pamoja  na  Wawakilishi kutoka Wizara ya Nishati na Madini, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Mamlaka ya Bandari Tanga . Pia yupo Meya wa Jiji la Tanga na Mkurugenzi wa Jiji la Tanga.
Maandalizi ya awali ya kuandaa eneo itakapojengwa Gati itakayotumika kupakua mafuta ghafi ya kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga yakiendelea.
Picha kwa Hisani ya www.tangaraha.tz.blogspot.com

Na Asteria Muhozya, Tanga.
Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Martine Shigella amesema, tayari Mkoa huo umeanza maandalizi ya awali ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga.

Shigella aliyasema hayo mwanzoni mwa juma alipotembelea eneo la Chongoleani Tanga itakapojegwa gati ya kushusha mafuta ili kuona maandalizi yanavyoendelea na kuongeza kuwa, Mkoa huo unaandaa mazingira ya kutekeleza mradi husika ambapo tayari barabara ya kuelea eneo hilo imekwishachongwa.

“Tunajenga mazingira ya kutekeleza mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi, lakini pia tunao wajibu wa kuboresha Bandari yetu kwa ajili ya utekelezaji huo. Yale tunayoweza kufanya sisi kama Serikali tayari tunaanza wakati tukisubiri Marais na Mawaziri wa nchi husika kusema ni lini ujenzi huu utaanza rasmi. Kwetu ni fursa na tunataka maendeleo.”

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Bandari ya Tanga, Henry Arika alisema kuwa, katika maandalizi ya mradi huo, Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) imetenga jumla ya Shilingi bilioni 9.2 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya bandari hiyo ili kuwezesha mapokezi ya vifaa vya mradi husika.

Aliongeza kuwa, mbali na kuboresha miundombinu, fedha hizo pia zitatumika kuongeza kina cha gati ili kuwezesha Meli kubwa zitakazobeba vifaa vya ujenzi kuweza kutia nanga kwa urahisi.

“TPA inatarajia kupokea wastani wa tani 250,000 za shehena za vifaa kupitia Bandari yetu wakati wa maandalizi na ujenzi wa bomba hilo, hivyo maboresho kwetu ni muhimu sana. Tunajua kazi kubwa iliyo mbele yetu, tunajipanga na tunajiandaa kuhakikisha kwamba mizigo inapita kwa ufanisi na usalama,” alisema Arika.

Alifafanua kuwa, ili kuimarisha usalama na kupanua wigo wa eneo la kuhifadhi mizigo, tayari Mamlaka hiyo imetenga eneo la ukubwa wa kilomita za mraba 2,600 litakalotumika kwa shughuli za kuhifadhia shehena ya mizigo kabla ya kusafirishwa, ikiwemo pia maandalizi ya ujenzi wa mashine maalum ya ukaguzi (scanner) kwa ajili ya kukagulia mizigo ili kuimarisha usalama.

Naye, Mkurugenzi wa Sheria kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Ibrahim Ngabo alisema kuwa, majadiliano ya mfumo wa Kisheria kuhusu mradi kati ya nchi za Tanzania na Uganda yamekwishaanza na yanaendelea vizuri.

Kwa upande wake, Kaimu Kamishna wa Nishati anayeshughulikia masuala ya Petroli, Wizara ya Nishati na Madini, Mwanamani Kidaya, alisema kuwa, amefurahishwa na namna Mkoa huo ulivyoanza maandalizi ya utekelezaji wa mradi husika na hivyo kuwataka wananchi kuwa tayari kuupokea mradi huo ikiwemo kutumia fursa zitakazojitokeza kupitia mradi husika.

Katika ziara ya kutembelea eneo hilo, Mkuu wa Mkoa alifuatana na Uongozi wa Mkoa akiwemo Meya  na Mkurugenzi wa Jiji hilo, Uwakilishi kutoka Wizara ya Nishati na Madini, TPDC na TPA.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad